01/06/2026
.
KITONKA MEDICAL YAWEKA KAMBI YA UCHUNGUZI WA BURE WA FIGO KWA WANANCHI
Katika kuendeleza sera yake ya kurudisha kwa jamii, Kitonka Medical Hospital tarehe 30 na 31 mwezi mei 2026 imeendesha kambi maalum ya uchunguzi wa bure wa magonjwa ya figo kwa wananchi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uelewa wa afya na kuhamasisha jamii kufanya uchunguzi wa mapema.
Kambi hiyo iliyovutia wananchi kutoka maeneo mbalimbali, iliambatana pia na huduma za uchunguzi wa presha, kiwango cha sukari mwilini pamoja na wingi wa damu, huduma ambazo zimeendelea kuwa muhimu katika kubaini mapema magonjwa yasiyoambukiza yanayoathiri idadi kubwa ya watu nchini.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, uongozi wa Kitonka Medical ulieleza kuwa lengo la kambi hiyo ni kusaidia wananchi kupata huduma za msingi za afya bila gharama, huku ukitoa elimu kuhusu umuhimu wa kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kuepusha madhara makubwa yanayoweza kujitokeza kutokana na kuchelewa kugundua maradhi.
Wananchi waliojitokeza walipongeza hatua hiyo wakieleza kuwa imewasaidia kufahamu hali zao za kiafya na kupata ushauri wa kitabibu kutoka kwa wataalamu waliokuwa kambini hapo.
Wataalamu wa afya walieleza kuwa magonjwa ya figo mara nyingi hayatoi dalili katika hatua za awali, hali inayowafanya watu wengi kugundulika wakiwa tayari katika hatua hatarishi.
Kutokana na hali hiyo, wananchi wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara, hasa kwa wenye historia ya presha, kisukari au matumizi ya muda mrefu ya dawa bila ushauri wa daktari.
Uchunguzi wa Figo Mara kwa Mara Huokoa Maisha