10/08/2026
Wazazi na walezi nchini wametakiwa kuwapeleka watoto wao wa k**e wenye umri wa miaka 9 hadi 14 kupata chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi ili kuwakinga dhidi ya ugonjwa huo unaoongoza kwa vifo miongoni mwa saratani za uzazi kwa wanawake.
Rai hiyo imetolewa leo na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) Frank Rutachunzibwa, wakati akitoa mada ya uelimishaji kuhusu saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha, Mtumba jijini Dodoma.
Dkt.Rutachunzibwa alisema chanjo hiyo hufanya kazi vizuri zaidi kwa watoto ambao bado hawajaanza kujamiiana kwani huwapa kinga dhidi ya maambukizi yanayoweza kusababisha saratani ya mlango wa kizazi baadaye katika maishani yao.
Alibainisha kuwa kila mwaka maelfu ya wanawake hupoteza maisha kutokana na saratani hiyo huku sababu kubwa ikiwa ni kuchelewa kugundua ugonjwa huo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali, Choto Sendo aliishukuru Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) kwa kutoa elimu ya magonjwa ya saratani na yasiyo ya kuambukiza kwa watumishi wa Wizara hiyo na kusema kuwa elimu waliyoipata pamoja na upimaji watakaofanyiwa utawasaidia kujua hali za afya zao.
Saratani ya mlango wa kizazi ni miongoni mwa saratani zinazoongoza kwa vifo vya wanawake nchini, huku changamoto kubwa ikiwa ni uelewa mdogo na kuchelewa kwa uchunguzi na matibabu. Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, chanjo kwa watoto wa umri wa miaka 9 hadi 14 ni njia muhimu ya kinga dhidi ya ugonjwa huo sambamba na uchunguzi wa mara kwa mara kwa watu wazima.