28/08/2026
WANAFUNZI WA SKILL PATH WAGEUZA WODI YA HOSPITALI YA SONGEA KUWA SEHEMU YA FURAHA
Si kila dawa huja kwenye chupa wakati mwingine, huja kupitia moyo wa mtoto.
Wanafunzi wa Skill Path English Medium Primary School ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wamefanya ziara ya kijamii katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, Songea, wakitoa zawadi na faraja kwa wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo.
Afisa Muuguzi Msaidizi aliyekuwa Msimamizi wa zamu, Sairice Mbena, alisema ziara hiyo imewapa wagonjwa faraja, matumaini na moyo wa kuendelea kupambana na changamoto za kiafya.
“Tunashukuru sana uongozi wa Skill Path kwa kufikiri kuwatembelea wagonjwa wetu,” alisema Mbena.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Skill Path English Medium Primary School, Rashidi Ayasi, alisema lengo la ziara hiyo ni kuwafundisha watoto upendo kwa vitendo, kuwajali wengine na kushiriki katika shughuli za kijamii.
Ziara hiyo inaonesha kuwa elimu bora si darasani pekee; inajenga pia kizazi kinachojua kuhurumia, kusaidia na kugusa maisha ya wengine.